Tuesday 25 March 2014

MKURUGENZI WA BODI YA ATALII AVULIWA MADARAKA

Filled under:



Serikali imemvua wadhifa Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi ya Utalii nchini (TTB), Dk Aloyce Nzuki kutokana na utendaji usioridhisha.

Akitangaza uamuzi huo jana mbele ya waandishi wa habari, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu alisema kuwa ameridhia uamuzi wa bodi ya wakurugenzi wa shirika hilo ambao walipendekeza mkurugenzi huyo aondolewe.
Katika barua waliyomwandikia Waziri ikiwa imesainiwa na Mwenyekiti wa Bodi, Charles Sanga na kuridhiwa na wajumbe wote, walidai Nzuki alishindwa kuutangaza utalii ambalo ndilo jukumu la bodi hiyo.

“Nilipata barua kutoka TTB ikinishauri kumwondoa Bwana Nzuki na baada ya kushauriana na naibu wangu na katibu mkuu nikaona ni vyema kukubaliana na ushauri wa bodi,” alisema Nyalandu jana, huku akiwa na naibu wake, Mahamoud Mgimwa na wajumbe wa Bodi ya TTB.
Nyalandu alisema Dk Nzuki atapangiwa kazi nyingine ndani ya wizara hiyo .
Aliwaomba Watanzania wenye uwezo kuomba nafasi hiyo hata wale walio nje ya nchi ili kuweza kusaidia kukuza utalii wa nchi, uwe mbele ya mataifa mengine duniani.
“Nategemea katika siku 21 nafasi hiyo iwe imezibwa, kwani nimewashauri watumie kampuni inayoheshimika ili kufanya mchakato huo ,” alisema.
Aliongeza kuwa baada ya mchujo kufanyika, bodi hiyo itampa majina ya watu watatu ambayo baadaye atayapeleka kwa Rais Jakaya Kikwete kwa ajili ya moja kuteuliwa kujaza nafasi hiyo.

0 comments:

Post a Comment