Tuesday 4 February 2014

ANGALIZO!!! JINSI NGONO YA MDOMO INAVYOLETA SARATANI YA KOO

Filled under:



Utafiti uliofanywa na Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini umeonyesha asilimia 20 ya saratani ya koo husababishwa na ngono ya mdomo maarufu kama ‘Oral Sex”.
Utafiti huo unaonyesha saratani ya koo licha ya kuambukizwa na njia mbalimbali ikiwemo ulaji wa vyakula vyenye pilipili, pombe kali, vitu vyenye uchachu pamoja na kurithi kutoka kwa wazazi. 
Utafiti unaonyesha watu wengi hasa vijana wanamejiingiza kwenye vitendo hivi vya kufanya ngono wakitumia midomo hasa  ndimi, hivyo kuhatarisha uhai wao.
Katika utafiti  huo wa hivi karibuni, ulibaini wanaume 747  na wanawake wakiwa 472 hugundulika kila mwaka kuwa na saratani hiyo huku wanaopoteza maisha kila mwaka ni wanaume 444 wakifuatiwa na wanawake 270 kutokana na ugonjwa huo.
Utafiti unabainisha kuwa asilimia kubwa ya vijana wenye umri kati ya miaka 20 hadi 45 wanatumia staili ya kuwanyonya wenza wao sehemu za siri lengo likiwa ni  kuwavutia wapenzi wao katika  kushiriki ngono.
Vijana  wenye umri huo ndio wahanga wakubwa kwa sasa kutokana na ugonjwa huo kuonekana kuwaathiri kwa kasi, huku wengi wakiwa hawajui athari zake. Baadhi hujisifia kwamba ni wajuzi, kumbe wanajitafutia kifo kwa kufanya vitendo hivyo.
Utafiti unaonyesha kwa watu wazima walio wengi hawana muda wa kufanya hayo wanayofanya vijana, hivyo kujikuta angalau wanakuwa salama na kupatwa na saratani ya koo kwa njia hiyo inayoonekana kama ni chafu pia.
Daktari  Bingwa wa Magonjwa ya Saratani kutoka Taasisi ya Saratani ya Ocean Road, Dk Crispin Kahesa anasema saratani ya  koo ni  ya pili katika mtiririko wa saratani zinazowapata wanaume  nchini, ikiongozwa na ile ya  ngozi (Karposi’s Sarcoma) ambayo huambukizwa kwa njia ya kujamiana. Kuna saratani aina zaidi ya 24 zinazoisumbua Tanzania.
Anasema mbali na staili hiyo pia, kuna baadhi ya watu hupata saratani ya  koo kwa kurithi kutoka kwa wazazi wao na wengine kuwa na  umri mkubwa ambao huchangia kupata tatizo hilo, lakini siyo kwa asilimia kubwa kama ile ya ngono ya mgomo.
“Hali hii ya vijana wenye umri huo kuwanyonya wanawake inatokana na ujana, wengine wanaiga kwenye mitandao, lakini mambo haya hayakuwepo zamani tofauti na sasa, utakuta wanaume ili aweze  kumvutia mwanamke anamfanyia hivyo sehemu za siri, lakini zamani staili hii haikuwepo kabisa,” anasema  Dk Kahesa na kuongeza.

“Kuna njia nyingi tu za kumvutia mwanamke lakini siyo hii bila kujua madhara yaliyopo, vijana wengi nchini wanaona njia rahisi ya kupendwa na mwanamke ni hiyo wakati kuna njia nyingi za kufanya. Nje ya hiyo wanawake wengine huwa na magonjwa mbalimbali, kwa jumla hakuna usalama wowote kwa wanaume kufanya kitendo hicho,”anaongeza

Sababu nyingine zaidi

Anasema staili ya maisha nayo imechangia kuongezeka kwa ugonjwa huo, vijana wengi kwa sasa hutumia muda mwingi  kuangalia video za ngono na staili zinazofanywa na wenzetu wa nje na hivyo kuongezeka kwa matumizi ya ngono ya mdomo.
Dk Kahesa anasema asilimia 12 ya wagonjwa wote wa saratani  nchini wanasumbuliwa na saratani ya koo, hivyo kuna kila sababu kwa vijana kubadilisha tabia na kuepuka kuiga mitindo ya wenzetu wazungu ambayo mara nyingi inapotosha mila na tamaduni za Kiafrika.
Anasema  katika mtiririko wa saratani zinazoongoza nchini saratani ya koo  inashika nafasi ya tano, wagonjwa wengi wanaopatwa na ugonjwa huo ni watu wenye umri mkubwa wa miaka 60 na kuendelea  hiyo inaonyesha kuwa wengi wao walianza  ngono ya mdomo muda mrefu wakati wakiwa  bado wadogo.

“Asilimia kubwa ya wagonjwa wanaopatikana na kansa ya koo nchini, inawapata  watu wenye umri wa kuanzia miaka 60 na kuendelea  kutokana na wengi wao kuanza mapema vitendo vya ngono kwa njia ya mdomo wakati  bado wadogo au wengine kurithi kutoka kwa wazazi wao,” anasema Dk Kahesa.

Aina ya kansa ya koo
Tafiti zinaonyesha kuna aina mbili za saratani ya koo; aina ya kwanza ni “Oesophagus Carcinoma na Squamous cell carcinoma, zote  hutofautiana wakati zinapimwa kwenye darubini lakini matibabu yake yanafanana.
Aina hizo ndizo zilizopo nchini na huanza mapema  kuharibu seli ambazo zipo katika  utandu uliopo katika ukuta wa koo kabla ya kuenea katika  maeneo mengine ya koo.

Visababishi vya kansa ya koo:
Moja kati ya vitu vinavyosababisha kansa ya koo ni mwenendo wa maisha yetu kwa kula vyakula vyenye  asidi, vyakula  vichachu, vyakula vyenye pilipili, pombe kali na  vyakula vigumu ambavyo hukwaruza koo na hivyo kusababisha saratani.
Anasema  asilimia 90 ya wagonjwa wanaopokelewa katika Taasisi ya Saratani ya Ocean road wanakuwa na  historia ya kutumia vikali kama pombe kali, kuvuta sigara kwa kupindukia, kula pilipili kwa wingi na kutumia vitu vyenye uchachu.

Dalili za saratani ya koo
Moja kati ya dalili za  mgonjwa wa saratani ni chakula kukwama kwenye koo, siku za mwanzo mgonjwa anaweza kushindwa kumeza chakula kigumu kisha cha majimaji na baadaye akashindwa kumeza hata mate.
Ugonjwa huo unachukua muda mrefu kugundua na kuona  viashiria kwani mwanzo  mgonjwa huanza kupata shida kumeza chakula na kwamba wagonjwa wengi wanaofika katika Taasisi hiyo ya Saratani wanakuwa tayari wamechelewa  kwani wanakuwa katika hatua ya mwisho.
“Unaweza usionyeshe dalili lakini kadri  siku zinavyokwenda  ndiyo kunakuwa na dalili zinajitokeza pia katika kipindi hicho mtu anakuwa na maumivu wakati wa kumeza chakula, maumivu katika kifua na mgongo  na hata kupungua uzito pamoja na kikohozi kikavu kinachoweza kudumu mwezi mmoja,” anasema.

Njia ya kuzuia saratani ya koo.
Kwanza mtu mwenye ugonjwa huo anapaswa kuhawi hospitali ili aanze matibabu mapema kutokana na ukweli kwamba mgonjwa anayewahi kupata matibabu ana uwezekano wa kupona kuliko yule ambaye amechelewa kugundulika na kuanza matibabu.
Kama  saratani hiyo itakuwa imeshambulia viungo  vyote vilivyopo jirani na koo na hadi kufika katika tezi  au kiungo kingine cha mwili, mgonjwa anaweza kutibiwa  kwa njia ya upasuaji, kutumia mionzi na hata kifaa maalumu ambacho ni kemikali.

Tafiti zilizofanywa nchini
Wataalamu mbalimbali nchi wamefanya tafiti zinazohusiana na ugonjwa huo na kusema kuwa kati ya mwaka 1983 hadi 1992 kulikuwa na kati ya watu 546 waliopimwa,  wanaume 430 na wanawake 116 waligundulika kuwa na ugonjwa huo.
Utafiti huo ulishirikisha watu  wenye  umri wa miaka 21 hadi 90, ulibaini kuwa wagonjwa wengi walikuwa wenye umri wa miaka 50-59 tofauti na hali iliyopo sasa ugonjwa wa kansa ya koo unawaathiri vijana wenye umri wa miaka 40.
Dk Kahesa anasema katika kipindi cha miaka saba iliyopita takwimu za taasisi yake imeongezeka kutoka kutoka wagonjwa 167 hadi kufikia wagojwa 277. Hali inaonekana huenda ikaongezeka kutokana na ukweli kwamba wengi wa watu wanaonekana kuendeleza tabia hatarishi zikiwemo hizo za kutumia midomo.

Magonjwa mengine sehemu za siri

Miongoni mwa magojwa ambayo yanaweza kumpata mtu ambaye ananyonya au kulambana sehemu hizo ni pamoja na gonjwa wa  gonoreha, ambapo ugonjwa huu huanzia katika koo na mwanzoni huhisi kama ni ukavu wa kifua au maradhi ya kawaida ya kifua, ila baadaye hushuka na kuelekea katika viungo vya uzazi.
Ugonjwa mwingine ni kaswende ambao huambukizwa kirahisi zaidi kupitia mdomo na hasa pale inapotekoa mdomo unapokutana na kiungo chenye athari hizo.
Vile vile ugonjwa wa chlamydia ni moja wapo kati ya magonjwa ya zinaa ambao huambukizwa kwa bakteria  na kwamba ugonjwa huu pia  huambukizwa kupitia mdomo, ingawa waathirika wanaweza wasijijue maana huwa hauna dalili kwa muda mrefu.
Hepatitis A: Hiki ni  ni kirusi kinachopatikana  katika kinyesi cha binadamu, kirusi hiki huwaingia wale wanaopenda kunyonya na kulambana sehemu za haja kubwa. Ni kwamba kwa ugonjwa huu mtu anaweza akaharibika macho hadi kupofuka.
Hepatitis B: Ugonjwa huu huambukizwa kama virusi vya Ukimwi kwa sababu virusi vyake hukaa katika majimaji yanayotoka katika sehemu za siri na damu. Mtu akiwa na ugonjwa huu, mwili wake unakuwa na vipele vingi na hata majipu ambayo huwa magumu kupona na wapo wanaokufa.
Vile vile ugonjwa wa Hepatitis C:  ni ugonjwa ambao hupatikana pindi damu inapotoka maana vijidudu vyake vinakaa katika damu. Ugonjwa huu humfanya mtu kuvimba viungo na hata kukatika.
Hata hivyo kupitia staili hii yaupeana raha kwa kunyonyana sehemu za siri, kuna uwezekano wa kupata maambukiz ya virusi vya Ukimwi kwa uchache lakini  kwa nchi zilizoendelea wamebuni aina ya kondom ambazo huvaliwa katika mdomo  wa binadamu na hivyo kupunguza hatari ya kupata madhara hayo.


JE NGUVU ZA KIUME ZINACHANGIA?
Dk Kahesa anasema  hakuna utafiti wa moja kwa moja unao onyesha kuwa baadhi ya wanaume wanaofanya ngono kwa njia ya mdomo wanakuwa na upungufu wa nguvu za kiume.
“Utafiti wa mtu mmoja hautoshi kuonyesha kuwa baadhi ya wanaume wanafanya ngono kwa njia ya mdomo wanakuwa na ukosefu wa nguvu za kiume, hivyo kinachotakiwa ni kufanya utafiti wa kina ili kubaini kama tatizo hilo lipo licha ya kuwepo kwa kesi nyingi zinazodaiwa kuwa baadhi ya wanaume hawana nguvu za kiume na wapenzi wao huwafichia siri kwa kufanya nao mapenzi kwa njia yam domo”anasema.

NINI KIFANYIKE:
Wataalamu wa masuala ya ndoa na saikolojia wanasema kuna njia nyingi za kuandaana wakati wa tendo la ndoa tofauti na kunyonyanyana sehemu za siri.

Wataalamu hao wanasema sio sahihi kwa mwanaume au mwanamke kunyonyana sehemu za ndoa mwenzake  na kwamba staili hizo  ni staili za wanzetu wa nje lakini kitu kinachosababisha kukua kwa kasi kwa staili hiyo ya kunyonyonyana sehemu za siri au kufanya mapenzi kwa njia ya mdomo ni kutokana na kasi ya  utandawazi.
Wadadisi wa mambo wanadai kuwa baadhi ya watu huiga staili hizo kutoka katika mitandao bila kujali kuwa kuna zina  madhara makubwa, hivyo ni jukumu la kila mtu kulinda afya yake na ya mwenza wake.
Sio kila kitu kinachowekwa katika mitandao ya kijamii  kina  manufaa la hashaa!  vitu vingine vinachangia kuhatarisha maisha.

0 comments:

Post a Comment