Thursday 30 January 2014

TFDA IMEINGIA KATIKA KASHFA BAADA YA KUMUAJIRI MTUMISHI ASIYE NA CHETI CHA TAALUMA YOYOTE.

Filled under:



MAMLAKA ya Chakula na Dawa Tanzania (TFDA) imeingia kwenye kashfa ya kumwajiri mtumishi asiye na cheti cha kitaaluma kuwa msaidizi wa maabara ya dawa kuanzia Desemba 2, 2013.

Mkurugenzi wa TFDA, Hiiti Sillo, jana alithibitisha kufanyika kwa udanganyifu huo lakini akafafanua kuwa baada ya kujiridhisha na tuhuma hizo, mtumishi huyo, Pilly Komba Kilongosi, amekabidhiwa barua ya kuachishwa kazi rasmi kuanzia Januari 28, 2014.

Uchunguzi wa gazeti hili ulibaini kuwa TFDA kupitia gazeti la serikali la Daily News la Julai 1, 2013 ilitangaza nafasi za kazi saba ikiwemo hiyo ya msaidizi wa maabara ya dawa ambapo mwombaji alitakiwa kuwa na sifa za elimu ya kidato cha nne na mwenye uzoefu usiopungua miaka mitatu katika kazi hiyo.

Vigezo vingine ni mwombaji kuambatanisha barua ya maombi, wasifu wake (CV), nakala za vyeti na hati ya matokeo (transcripts), picha mbili za pasipoti na majina ya wadhamini wawili.

Vyanzo vyetu vilibaini kuwa Pilly alituma barua ya maombi Julai 5, 2013, akionyesha kuwa amehitimu kidato cha nne katika Sekondari ya Temboni jijini Dar es Salaam na kisha kuhudhuria kozi ya msaidizi wa maabara ngazi ya III na II katika Chuo cha Veta cha Dar es Salaam mwaka 2011/2012.

Katika barua hiyo, Pilly anadai kuwa anao uzoefu katika kazi hiyo kwa zaidi ya miaka mitatu akifanya kazi kama mfanyakazi wa muda TFDA na TBS wakati ukweli ni kwamba amefanya mafunzo kwa vitendo kwa miezi 12 pekee yaani TFDA mizei tisa na TBS miezi mitatu.

Pilly aliongeza kuwa ameambatatisha nakala za vyeti kikiwemo kile cha kidato cha nne ambacho hana kutokana na kupata daraja sifuri katika mtihani wake wa mwisho, CV na hati ya matokeo ya kitaaluma.

Katika hatua inayotia shaka kwamba Pilly aliandaliwa mapema kupewa ajira hiyo, majukumu saba yanayotajwa katika tangazo kwa mwombaji kuyajua, ndiyo hayo hayo yameorodheshwa na Pilly katika CV yake neno kwa neno kuanzia namba moja hadi saba.

Kwa mujibu wa vielelezo ambayo gazeti hili linavyo, Pilly alihitimu kidato cha nne mwaka 2010, ambapo alifanya mtihani kwa namba S3799/0098 na kupata daraja sifuri la alama 35 akiwa amepata F katika masomo yake yote ya Uraia, Historia, Jiografia, Kiswahili, Kiingereza, Baiolojia na Hesabu.

Pamoja na kukosa vigezo tajwa, Pilly aliajiriwa kama mtumishi wa TFDA tangu Desemba 2, 2013 hadi Januari 28, 2014, alipofukuzwa baada ya kubainika alipenyezwa kinyemera.

Alipohojiwa Mkurugenzi wa TFDA kuhusu hatua zilizochukuliwa kwa waliofanya udanganyifu huo, alisema kuwa hizo ni taratibu za ndani za utumishi ambazo zinaendelea kufanyika.

“Ni kweli huyo binti aliajiriwa kwetu lakini kama unavyosema baada ya kufanyika uchunguzi tulibaini makosa yalifanyika wakati wa mchakato wa usaili, hivyo jana amepatiwa barua ya kuachishwa kazi rasmi na amehojiwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU),” alisema Sillo.

Akizungumza na gazeti hili kuhusu madai hayo, Pilly alithibitisha kupewa barua ya kuachishwa kazi juzi akielezwa kuwa alikosa sifa ya kutokuwa na cheti cha kitaaluma cha kidato cha nne na kwamba alihojiwa pia na TAKUKURU ili kutoa maelezo.

“Alipoulizwa alipataje kazi wakati hakuwa na vigezo, Pilly alijitetea kuwa: “Kazi zilitangazwa nikaomba na nikapata, hivyo siwezi kujua vigezo gani walitumia katika mchakato wa usaili”.

“Alipoulizwa alipataje kazi wakati hakuwa na vigezo, Pilly alijitetea kuwa: “Kazi zilitangazwa nikaomba na nikapata, hivyo siwezi kujua vigezo gani walitumia katika mchakato wa usaili”.

0 comments:

Post a Comment