Wednesday, 22 January 2014

NYARANDU AANZA NA WATUMISHI WALIOIDHALILISHA WIZARA

Filled under:


Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu ameingia ofisini kwa mara ya kwanza jana baada ya kuapishwa juzi na Rais Jakaya Kikwete huku akitangaza kuanza na watumishi wote walioidhalilisha Wizara ya Maliasili na Utalii kwa kujihusisha kwa njia moja ama nyingine na majangili.

Nyalandu aliyepandishwa kuwa waziri kamili baada ya kujiuzulu kwa aliyekuwa akiishika nafasi hiyo, Balozi Khamis Kagasheki akizungumza jana alisema, kwa mara ya kwanza lazima taswira nzuri ya wizara ionekane na kitakachofanyika ni kuwashughulikia watumishi wasio waaminifu.
Akiwa ameambatana na Naibu Waziri wake, Mahmoud Mgimwa, Nyalandu alisema, watumishi wa wizara hiyo watakaoonekana kwenda kinyume cha utendaji kazi na kuchafua taswira ya wizara yake, watachukuliwa hatua kali ikiwa ni pamoja na kutimuliwa kazi.
“Harakati za kupambana na majangili itakuwa ndiyo kaulimbiu yangu na mwenzangu,” alisema Nyalandu.
Alisema kwa kuanzia, wizara yake inawasaka watu watatu waliohusika na kuua faru na kuchukua pembe zake katika Hifadhi ya Taifa ya Serengeti mkoani Mara.
Waziri Nyalandu akitoa taarifa za kuuawa kwa faru huyo Jumamosi iliyopita alisema, faru huyu aliuawa na majangili usiku huo.
“Hifadhi ya Serengati ina faru 32 pamoja na faru watano walioletwa na mradi maalumu, unaosimamiwa na Rais Jakaya Kikwete kutoka Afrika Kusini, ila faru mmoja kati ya hao watano aliuawa mwaka juzi.”
Jana Nyalandu alisema, katika kupambana na ujangili wamekamilisha rasimu ya awali ya kubadili Idara ya Wanyamapori kuwa Mamlaka ya Wanyamapori Tanzania itakayosaidia kuinua morali ya wafanyakazi ili wafanye kazi za kupambana na majangili katika mazingira yenye hatari nyingi katika maisha yao.
Kwa upande wake Mgimwa alisema, watafanya kazi kwa bidii na ushirikiano wa karibu ili kuhakikisha kuwa wizara hiyo inakuwa ya kwanza na ya mfano katika Mpango wa Serikali wa Matokeo Makubwa Sasa (BRN) kwa kuhakikisha sekta ya utalii inachangia zaidi ya asiliamia 23 ya pato la taifa kwa mwaka.

0 comments:

Post a Comment