Thursday 17 April 2014

LUKUVI ALIKOROGA KWA CUF

Filled under:

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, amekiri kutoa maneno yanayodaiwa kuwa ya uchochezi kanisani kwa madai ya kuingiwa hofu na harakati za asasi ya kidini ya Uamsho, kufanana na za Chama cha Wananchi (CUF) za kudai Serikali ya mkataba.

Waziri Lukuvi alitoa kauli hiyo jana bungeni, akitoa ufafanuzi wa kauli aliyopata kuitoa katika Kanisa la Methodist wakati wa kumsimika Askofu Mteule, Joseph Bundara.

Katika misa hiyo, Lukuvi aliwaambia waumini wa kanisa hilo kwamba muundo wa serikali tatu utavunja Muungano na ikipitishwa, jeshi litaingilia kati kuongoza nchi, kauli ambayo juzi ilisababisha UKAWA wasusie Bunge.

Katika ufafanuzi wake jana bungeni Lukuvi alikiri kutoa kauli hiyo kanisani kwa madai ya kuingiwa hofu ya kutokea ubaguzi wa kidini.

Alisisitiza kuwa hofu yake inatokana na harakati zinazofanywa na kikundi cha  Uamsho visiwani Zanzibar, kufanana na za CUF ambazo ni kudai Serikali ya Mkataba.

Alisema uamsho imekuwa ikihusishwa na vurugu zinazotokea mara kwa mara visiwani humo, zinazohusishwa na vuguvugu la kudai mamlaka kamili ya Zanzibar.

Akitolea mfano, Lukuvi alisema Mwenyekiti wa Bunge hilo, Samuel Sitta,  alipotumwa Zanzibar kupeleka Rasimu ya Katiba, rasimu hiyo ilichukuliwa na wanauamsho na kuichanachana, kisha kuisigina mbele yake.
“Sasa niwaulize humu ndani…Uamusho ni nani…?”  Wajumbe kwa wingi wao na vigelegele wakajibu  “Ni CUF”. Akauliza mara ya pili: “Uamusho ni nani…?” akajibiwa: “ CUFUUUUU”.

“Lakini kuna swali liliulizwa hapa bungeni, CUF wakaja juu wakasema ni Taasisi ya Kidini…sasa unaniambiaje mimi nisiwe na hofu ya kidini wakati kuna chama cha siasa kinahusiana na Uamsho lakini ina ladha ya kidini.

“Na kwa kuwadhihirishia hivyo,  kila mara CUF na Uamsho utakapomtaja  Mwalimu Nyerere na kumtaja Karume wanakwambia alaaniwe.. lakini hizi ndiyo sera za hao mnaowasema, sasa tunakuwaje na chama cha siasa ambacho tayari kinajipanga kutawala Zanzibar, lakini kinaendeshwa na Sera za Uamsho…uamsho wenyewe wanasema ni Taasisi ya Kidini, kwa nini usiwe na wasiwasi na mihemko yote ile ya Uamsho mpaka na Bara tukatikishika, kwa nini tusiwe na wasiwasi kwamba CUF ikichukua nchi basi Uamsho ndiyo 
utatawala, kwa nini tusiwe na hofu, yametokea na sisi tumeyaona, kwa nini wanajificha kwenye kivuli cha dini ili kufanya siasa…na kwa nini dini imetumika vizuri sana kueneza sera za CUF za serikali tatu, na kila wachosema CUF ndicho wanachosema uamsho?,”  alihoji Lukuvi.

“Na ukishaona chama kinajitayarisha kuchukua madaraka kama ilivyo kwa CUF, kinatumia taasisi hii yenye msimamo mkalii kueneza sera zake ni hatari kwa mustakabali wetu, ni hatari kubwa,” alisema.
Alisema kama kweli Uamsho ni taasisi ya kidini na inatekeleza sera ambazo zinatekelezwa na vyama vya siasa, lazima Watanzania wajiulize kuna nini.

Alisema kuna tishio la baadhi ya watu ambao wameanza kufikiria kwamba Wazanzibar wanafaidi sana wakiwa Tanzania Bara na kufikiria kuwafukuza na kunyang’anya mali zao na iwapo watafanikiwa kuwanyang’anya watawafukuza.

“Sasa baada ya Wazanzibari kuondoka, tutaanza kuangalia hawa Wachina, hawa Wahindi na vinginevyo tutakuja hata kwenye dini, Wakristo wana mali zaidi kuliko Waislamu.Lakini kwa Zanzibar ambayo ina dini kubwa moja na tunajua hizi dini, kwa mfano katika dini ya Ukristo kuna dini ndogo ndogo nyingi na ndani ya ukristo kuna watu wenye siasa kali lakini na ndani ya Uislamu kuna watu wenye siasa kali kwa hiyo mimi nina hofu nyingine ya ubaguzi .
 
“Nasema kunaweza kukatokea ubaguzi wa kidini, inaweza ikatokea ubaguzi wa kieneo kwani inaweza kutokea hata Unguja akaenda mtu akasema Waunguja wote ondokeni hapa pamejaa, sasa hizi ni hofu zangu, mfumo huu wa serikali mbili umetuondolea hofu hizi hatuna hofu kabisa ya maisha haya, leo hatumfikirii Mpemba atoke au Muunguja atoke, Msukuma atoke, hatufikirii,” alisema.

Awali kabla ya Lukuvi kutoa ufafanuzi huo, Sitta aliwaambia wabunge kuwa amemlazimisha Lukuvi kukatiza safari yake nchini India ili atoe ufafanuzi wa kauli alizozitoa katika Kanisa la Methodist.

Alisema amelazimika kumwita Lukuvi ambaye alikuwa akijiandaa kuondoka nchini jana kwenda India kwa matibabu ili atoe ufafanuzi wa kauli yake ambayo juzi ilisababisha UKAWA, wanaounga mkono serikali tatu, kususia Bunge hilo.

Moto wa wajumbe wa UKAWA, kutoka bungeni juzi uliwashwa na Profesa Ibrahim Lipumba ambaye alisema serikali na mawaziri wake wameanza kampeni ya kupinga muundo wa serikali tatu unaopendekezwa na rasimu ya Katiba iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.

Alisema hoja ya Lukuvi inafanana na ile ya Rais Kikwete aliyoitoa wakati wa kufungua Bunge, Machi 21, mwaka huu.

Tanzania Kwanza wamruka Lukuvi
Wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba wanaojiita Tanzania Kwanza, wamemruka Mjumbe wa Bunge hilo, William Lukuvi, kuwa kauli aliyoitoa kanisani na kusababisha mtafaruku ndani ya bunge ni maoni yake binafsi na si maoni ya serikali ya CCM.

Akitoa ufafanuzi jana, Kiongozi wa kundi hilo, Adam Malima, alisema Lukuvi kama mjumbe ana uhuru wa kutoa maoni yake na kwamba aliyoyasema ni yake na wala si ya chama wala serikali.
Kuhusu kauli za matusi, Malima alisema haoni kama kuna matusi na kuongeza kuwa tusi kubwa ni lile alilolitoa Profesa Lipumba kwamba  wote wanaodai serikali mbili ni Interahamwe.


0 comments:

Post a Comment