Monday 14 April 2014

KITUO CHA MABASI CHALIPULIWA

Filled under:



Watu kadha wameripotiwa kuuawa nchini Nigeria kutokana na milipuko miwili iliyotokea katika kituo cha mabasi katika mji mkuu wa Nigeria, Abuja.
Mwandishi wa BBC mjini Abuja, Haruna Tangaza anasema milipuko hiyo ilitokea wakati abiria wakiwa katika harakati za kupanda mabasi na teksi wakienda maofisini katikati ya mji wa Abuja.

Watu walioshuhudia tukio hilo wanasema miili ya watu imetapakaa katika eneo la tukio.
Waandishi wa habari wanasema huenda tukio hili ni shambulio la kikundi cha wapiganaji wa Kiislam kijulikanacho kama Boko Haram.

Mmoja wa walioshuhudia mlipuko huo, Badamsi Nyanya ameiambia BBC kuwa ameona miili 40 ikiondolewa. Watu wengine walioshuhudia tukio hilo wanasema wamewaona wafanyakazi wa uokoaji na polisi wakiokota sehemu za miili zilizotawanywa na milipuko hiyo.

Mlipuko huo ulichimba chini mita 1.2 katika viwanja vya Nyanya Motor Park, kiasi cha kilomita 16 kutoka katikati ya jiji, na kuharibu zaidi ya magari 30, na kusababisha mlipuko zaidi kutokana na matangi ya mafuta ya magari hayo kushika moto na kuwaka.
Magari ya wagonjwa yamekuwa yakibeba miili ya watu waliokufa na wale waliojeruhiwa katika hospitali za karibu.

Shuhuda mwingine Bi Mimi Daniels, ambaye anafanya kazi mjini Abuja, anasema: "nilikuwa nasubiri basi niliposikia mlipuko mkubwa halafu nikaona moshi," ameiambia Reuters.
"Watu walikuwa wakikimbia ovyo kutokana na taharuki."

0 comments:

Post a Comment