Saturday, 18 January 2014

MGOGORO ULIOPO NDANI YA KANISA LA MORAVIAN UNATOKANA NA UCHU WA MADARAKA

Filled under:



KANISA la Moravian kupitia Kamati yake ya Mpito ya Jimbo la Misheni Mashariki imemwandikia barua Msajili wa Vyama na Taasisi za Dini aliyepo Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kupuuza taarifa alizopewa za Mkutano Mkuu wa Taifa uliofanywa na kundi lenye mgogoro katika kanisa hilo.

Mkuu wa Mawasiliano, Mahusiano, Uandishi na Uratibu wa kanisa hilo, Mchungaji Emmaus Mwamakula, alisema hayo jana alipozungumza na waandishi wa habari kuhusu mkutano huo batili uliofanyika Desemba 26 hadi 28, mwaka jana ambao ulitolewa tamko na Askofu wa Jimbo la Kusini, Lusekelo Mwakafwila.

Alisema walimtaka msajili huyo kurejea maelezo ambayo wamekuwa wakimpa kwa njia ya e-mail pamoja na nyaraka mbalimbali walizompatia kutoka uongozi wa Kanisa la Moravian duniani kuhusiana na mgogoro wa kanisa katika jimbo hilo.

Mwamakula alisema mgogoro uliopo katika kanisa hilo unatokana na uchu wa madaraka kwa baadhi ya viongozi ambapo Mwakafwila na wenzake walibuni tuhuma za uongo dhidi ya Mwenyekiti wa Jimbo hilo, Mchungaji Clement Fumbo, kwa lengo la kumchafua pamoja na watendaji wengine, jambo ambalo wameshindwa kulithibitisha mpaka sasa.

“Tunapenda kuifahamisha ofisi yako kuwa mkutano mkuu ulioitishwa na Askofu Lusekelo Mwakafwila ni batili kwa mujibu wa kanuni na taratibu za Kanisa la Moravian na hivyo uongozi uliochaguliwa kutokana na mkutano huo ni batili,” alisema.

Alisema pamoja na uongozi wa Moravian duniani kumpa nafasi ya kusuluhisha jambo hilo Askofu Mwakafwila, bado alivuruga kwa makusudi hatua muhimu zilizokuwa zimefikiwa za kupatanisha kanisa hilo.

Alitoa wito kwa viongozi wa kanisa hilo na hata wale wa madhehebu mengine ya Kikristo kukemea kwa nguvu vitendo vya kuchochea fujo ndani ya nyumba za ibada.

0 comments:

Post a Comment