Friday 29 November 2013

MALAWI NA TANZANIA YAWASILISHA USHAHIDI WA UMILIKI WA ZIWA NYASA

Filled under:



                               Mwisho wa mpaka wa ziwa nyasa


Malawi na Tanzania zimewasilisha ushahidi na majibu ya maswali kuhusu umiliki wa maeneo kwenye Ziwa Nyasa, kwa jopo la wasuluhishi linaloongozwa na Rais mstaafu wa Msumbiji Joachim Chissano.

Wasuluhishi hao walizitaka Malawi na Tanzania kutoa majibu ya maswali manne muhimu, wakati wakiwasilisha ushahidi wao kuhusu umiliki wa ziwa hilo wenye mgogoro.
Mgogoro huo uliibuka baada ya Serikali ya Malawi bila kushauriana na Tanzania kutoa leseni kwa kampuni mbili za kigeni, kutafuta mafuta katika eneo la ziwa ambalo linamilikiwa na Tanzania.

Kwa mujibu wa gazeti la mtandaoni la Malawi la  Nyasa Times, msemaji wa Waziri wa Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa wa Malawi, Quent Kalichero alithibitisha Jumatano wiki hii kwamba nchi hiyo imewasilisha majibu ya maswali hayo na ushahidi uliohitajika.

“Waziri wetu amewasilisha taarifa maalumu ya maandishi kwa wasuluhishi na kwa sasa yuko nchini Msumbiji, kwa ajili ya suala hilo,” alisema Kalichero juzi.
Makabidhiano hayo yalifanyika mjini Maputo, Msumbiji ikiwa ni siku chache baada ya Rais Jakaya Kikwete kufanya mazungumzo na wasuluhishi, marais wa zamani wa Msumbiji, Joachim Chissano na wa Botswana, Festus Mogae jijini Dar es Salaam.

Akizungumza baada ya mkutano huo wa Jumatatu mjini Dar es Salaam, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Tanzania, Bernard Membe aliwaeleza wanahabari kwamba mazungumzo baina ya Rais Kikwete na wasuluhishi hao yalihusu zaidi ushahidi wa Tanzania katika suala la umiliki wa Ziwa Nyasa.
Pia alithibitisha kwamba Tanzania ilikuwa tayari  kuwasilisha ushahidi wake kwa sekretarieti ya ofisi ya waliokuwa wakuu wa nchi za Jumuiya ya Maendeleo ya Kusini mwa Afrika (SADC) inayoongozwa na Chissano, Jumatano iliyopita.

Baada ya mkutano huo wa Jumatatu, Membe alieleza kwamba nchi zote husika, yaani Tanzania na Malawi zinatakiwa kuheshimu maagizo na kuwasilisha ushahidi huo kwa wakati, na kuwaachia wasuluhishi kazi ya kupitia na kutekeleza wajibu wao wakiwa wamepewa muda unaofikia mwaka mmoja kupata suluhu.

Wasuluhishi hao wa SADC, Chissano na Mogae waliwasili jijini Dar es Salaam Jumapili iliyopita kwa ajili ya mazungumzo kuhusu mgogoro huo, kama walivyofanya kwa Malawi Julai mwaka huu.
Julai mwaka huu, Rais Joyce Banda wa Malawi alinukuliwa akisema kuwa nchi yake haina nia ya kulegeza kamba katika mgogoro wa mpaka wa Ziwa Nyasa na Tanzania.

Alitoa msimamo huo baada ya kukutana na Chissano wa Msumbiji na Thabo Mbeki wa Afrika Kusini ambao ni wajumbe maalumu wa Jumuiya ya SADC katika mgogoro huo.

0 comments:

Post a Comment