Wednesday, 22 January 2014

NAPE NAUYE APATA WAKATI MGUMU BAADA YA KUSALITIWA

Filled under:



KATIBU wa Halmashauri Kuu (NEC) ya Chama Cha Mapinduzi (CCM), Nape Nnauye, amepoteza uhalali wake wa kuendelea kushika wadhifa huo, kutokana na utendaji wake kukinzana na Mwenyekiti wake, Rais Jakaya Kikwete
 
Hali hiyo inatokana na taswira inayozidi kujitokeza kati ya wawili hao katika kusimamia masuala mazito yaliyoasisiwa na chama hicho.

Kwa nyakati tofauti, umejitokeza msigano ambapo wakati Nape akizunguka kwa wananchi mikoani kunadi msimamo wa CCM kuhusu jambo fulani, Rais Kikwete baadaye anajitokeza na kutoa mtazamo tofauti.

Hatua hii imeibua mkanganyiko kwa wananchi, na hivyo baadhi kufikia hatua ya kushauri Nape aachie ngazi ili kuonyesha kuwa amesalitiwa badala ya kuendelea kuonekana adui kwa wale anaosimamia wang’olewe.

Mhadhiri mwandamizi wa Chuo Kikuu cha Bukoba, Dk. Azavery Lwaitama, alizungumzia hali hiyo akisema inaonyesha kuwa hakuna mawasiliano kati ya Rais Kikwete na sekretarieti yake ya chama.

Alisema kuwa kama kungekuwa na mawasiliano ya kutosha, rais asingewateua tena baadhi ya mawaziri waliodaiwa na chama chake kuwa mizigo kuendelea kushika madaraka.

Mwishoni mwa mwaka jana, wakiwa katika ziara za kuimarisha chama mikoa ya Nyanda za Juu Kusini, Nape mbele ya Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahman Kinana, aliwataja baadhi ya mawaziri akiwaita mizigo kutokana na kushindwa kuwajibika ipasavyo.

Katika mikutano yao tofauti ya hadhara, Nape alikwenda mbali zaidi akisema mawaziri hao lazima waitwe mbele ya Kamati Kuu ya chama kujieleza na kuchukuliwa hatua.

Mawaziri waliotajwa ni Christopher Chiza (Kilimo na Chakula) na Naibu wake, Adam Malima, Dk. Shukuru Kawambwa (Elimu na Mafunzo ya Ufundi) na Prof. Jumanne Mghembe (Maji)

Lakini kama hiyo haitoshi, katika kikao cha wabunge wa CCM na Rais Kikwete mjini Dodoma mwaka jana, mawaziri Dk. Mathayo David (aliyekuwa wa Mifugo na Maendeleo ya Uvuvi) na Kawambwa walidaiwa kupwaya na kutakiwa kuondolewa ili kunusuru chama.

Pia vikao vilivyopita mwaka jana, Bunge likiongozwa na wabunge wa CCM walimtaja Waziri Mkuu Mizengo Pinda na Waziri wa Tamisemi, Hawa Ghasia pamoja na naibu wake Agrey Mwanri kama mizigo kwa kushindwa kukomesha ufisadi kwenye halmashauri.

Katika hatua ya kushangaza, Rais Kikwete katika mabadiliko ya baraza lake hivi karibuni, aliwarejesha mawaziri wote watuhumiwa isipokuwa Dk. Mathayo aliyeng’oka kwa shinikizo la Bunge.

Kurejeshwa kwa mawaziri hao kumeibua mjadala mkali kwa wananchi, huku wengi wakihoji ni kwanini rais hafanyi mawasiliano na chama chake ili kuondoa chuki zinazoweza kujitokeza
 
Hii si mara ya kwanza kwa Rais Kikwete kusigana na CCM, kwani hata wakati wa utekelezaji wa falsafa ya kujivua gamba iliyoasisiwa mwaka 2011 na kusimamiwa na sekretarieti, baadaye ilishindwa kutokana na msimamo wa mwenyekiti huyo.

Itakumbukwa kuwa baada ya falsafa hiyo kuasisiwa, Nape na Naibu Kaibu Mkuu wa CCM (Bara) wakati huo, John Chiligati, walizunguka mikoani wakijiapiza kuwa watuhumiwa wa ufisadi lazima wang’oke ndani ya siku 90.

Hadi muda huo unamalizika, ni mtuhumiwa mmoja pekee, Rostam Azizi, aliyekuwa mbunge wa Igunga ndiye aliyejiuzulu huku akiwatuhumu Nape na Chiligati kuwa walipotosha dhana nzima.

Nape aliwataja Rostam, Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa na Mbunge wa Bariadi Magharibi, Andrew Chenge, kuwa ni miongoni mwa wanaotakiwa kujivua gamba.

Pia aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa CCM (Tanzania Bara), Pius Msekwa, alithibitsha baadaye kuwa alikutana na Chenge, Lowassa na Rostam na kwamba taarifa ya matokeo ya mazungumzo itawasilishwa katika vikao vikuu vya chama.

Hata hivyo, baadaye kwenye kikao cha Kamati Kuu (CC), Rais Kikwete alisema kuwa dhana hiyo ilipotoshwa na kuonekana iliwalenga baadhi ya watu, jambo alilosema halikuwa kweli.

Kwa msimamo huo, Lowassa, Chenge na watuhumiwa wengine walijiona washindi na hivyo Nape na sekretarieti yake kutafsiriwa kama viongozi waliokuwa wakiendesha siasa za chuki ndani ya chama.

Tangu wakati huo, yamejengeka makundi ndani ya chama ambayo kwa kiasi fulani yanamwona Nape na sekretarieti kama wafitini wanaojitwika jina la mwenyekiti kuwashughulikia wengine.

Kwa hivyo, hata uamuzi wa Rais Kikwete kuwarejesha baadhi ya mawaziri waliodaiwa na sekretarieti kuwa mizigo, unaelezwa kwamba huenda ukaibua chuki kati ya mawaziri na Nape.

“Hivi hata ungekuwa wewe ni Nape, unapata wapi uhalali wa kuendelea kuongoza watu ambao mwanzo uliwaona hawafai kiutendaji, lakini sasa wamerejeshwa na mkuu wakof?

“Hawa kwa vyovyote watamjengea Nape na sekretarieti yake chuki. Vile vile watamdharau kama kiongozi wao kwa sababu ni mara ya pili sasa anasigana na mwenyekiti wake,” alisema mwenyekiti wa CCM wa mkoa ambaye aliomba kuhifadhiwa jina.

Hatua ya Rais Kikwete kuwateua watuhumiwa haiishii ndani ya CCM pekee bali hata baadhi ya wabunge walidai kushangazwa na uteuzi wa Mbunge wa Mbozi Mashariki, Godfrey Zambi, kuwa Naibu Waziri wa Kilimo na Chakula wakati bado anatuhumiwa kuomba rushwa.

Juni 13, 2011, Mbunge wa Kigoma Kusini (NCCR Mageuzi), David Kafulila, aliwataja wabunge wawili wa CCM bungeni akidai waliomba rushwa katika halmashauri ambayo hakuitaja.

Akichangia mpango wa maendeleo wa miaka mitano, Kafulila aliwataja Zambi na Mbunge wa Bahi, Omary Badwel akidai kwamba aliwakamata wakiomba rushwa kwa viongozi wa halmashauri.

Hadi sasa tuhuma hizo zimekaliwa na ofisi ya spika, huku Kafulila akisisitiza kuwa kile alichokisema ni ukweli mtupu na kwamba ushahidi wake alishaukabidhi, lakini anashangazwa na ukimya uliopo.

Baada ya Kafulila kuibua tuhuma hizo, Badwel alikumbwa tena na kashfa nyingine baada ya kukamatwa na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), akidaiwa kuomba rushwa kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Bagamoyo.
Hivi sasa mbunge huyo anaendelea na kesi yake katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

0 comments:

Post a Comment