Wednesday, 22 January 2014

MAJANGA YAMKUTA RPC TARIME BAADA YA KUMNYANYASA ASKARI WAKE

Filled under:


KAMANDA wa Polisi Kanda Maalumu ya Tarime Rorya, Justus Kamugisha, anatumia madaraka yake vibaya kumnyanyasa askari wake, G. 2751 PC. Japhet Samwel, aliyeumia mkono akiwa kazini mgodini Nyamongo. 

Licha ya kumnyima fedha za matibabu na hivyo kumsababishia ulemavu wa mkono wake, kamanda huyo sasa amefikia hatua ya kutaka kumuhamisha kwa nguvu kwenda mkoani Mwanza kuanzia Januari 20, mwaka huu.

Samwel ambaye mkono wake hauwezi kufanya kazi kwa sasa, na hivyo kushindwa kuisaidia familia yake, alikuwa ni miongoni mwa askari 31 waliopelekwa mgodini Nyamongo wakitokea mjini Tarime kuanzia Septemba 30 hadi Desemba 25, mwaka jana.

Taarifa hizo zilifichuliwa kwa mara ya kwanza na gazeti hili mwaka jana, hatua iliyosababisha Makao Makuu ya Jeshi la Polisi kuingilia kati kuchukua hatua, juhudi ambazo hata hivyo zimeyeyuka sasa.

Kwa mujibu wa vyanzo vyetu, baada ya askari huyo kutishia kuacha kazi, aliyekuwa IGP, Said Mwema, alimtuma kamishna msaidizi wa makao makuu, Shumbusi, aliyefika Tarime na kuonana na Samwel.

Gazeti hili lilidokezwa kuwa Samwel alimweleza Mshumbusi kuwa anataka alipwe gharama zake za matibabu na endapo jeshi halina fedha kama alivyoelezwa, basi apewe likizo ya kujitibia mwenyewe.

“Sikupewa fedha hiyo ya matibabu, badala yake nilipewa likizo ya miezi mitatu na baada ya kurejea kazini kama wiki nne zilizopita, nilipangwa kufanya kazi ofisi ya OC CID.

“Pale niliwekwa kama kujifunza kazi maana mkono wangu huu kwa sasa siwezi kufanya kazi yoyote ngumu,” alithibitisha Samwel baada ya kuulizwa juzi.

Alisema hivi karibuni alifika kamishna msaidizi mwingine wa makao makuu, Gerald, na kukutana na askari wote wanne walioathirika katika tukio hilo ili kuzungumza nao kuhusu fidia zao.

Kwa mujibu wa chanzo chetu, askari hao walihoji ni kwanini wanaambiwa kuwa wanaweza kulipwa fidia ndogo kuliko madhara waliyopata, na kuliko gharama walizotumia kujitibia ilhali waliumia wakiwa kazini.

Kwamba walielezwa kuwa wasingeweza kulipwa fedha hizo kwa vile wana bima ya afya, jambo walilodai ni kinyume na Police Regulation Act ya 2010 kwani bima ya afya haigharamii nauli, chakula wala malazi.

Akizungumza na gazeti hili, Samwel alikiri kufanya kikao na kiongozi huyo wa makao makuu akiwa pamoja na Kamanda Kamugisha, akisema kuwa alishangaa kuona kesho yake akiletewa fomu ya uhamisho.

Januari 17, mwaka huu, Samwel alipokea movement order iliyosomeka; Umeamriwa kuondoka hapa kikosini kwenda Ofisi ya Kamanda (M) Tarime Rorya. Kwa maelekezo zaidi piga timamu kwa Staff Officer kwa maelekezo ya kutekeleza amri ya uhamisho kwenda Mwanza. Simu kumb TRR/AD.21/189 yahusika.”

Baada ya kupewa fomu hiyo, alikwenda kuhoji anakwendaje Mwanza bila kupewa fedha za uhamisho na kujikimu kwa familia yake, lakini akajibiwa na Kamishna Sweetbert Henjewele kuwa suala la familia wao haliwahusu.

Januari 20, mwaka huu, aliletewa movement order nyingine ikisomeka; “Umeamriwa kuondoka hapa terehe 20/1/2014 kwenda Mwanza kwa ajili ya kutekeleza amri ya uhamisho wa Inspekta Jenerali wa Polisi. Ufikapo huko utaripoti kwa RPC Mwanza kwa maelezo zaidi. Simu PHQ/AD.21/VOLXXI/267 ya tarehe 16/07/2013 yahusika”.

Samwel alisema: “Mimi nimekataa kuichukua hiyo fomu kwa sababu sina nauli ya kwenda Mwanza na isitoshe sijajua fanilia yangu inabakije hapa kama nalazimishwa kwenda tu huko tena kwa vitisho vya kuadhibiwa kijeshi.”

Mwandishi liliwasiliana na Kamanda Kamugisha ili kufahamu ni kwanini askari huyo hapewi haki yake, ambapo alisema hana taarifa ya suala hilo.

Alipoulizwa kuwa anamchukia Samwel kwa sababu alivujisha suala hilo kwenye vyombo vya habari, alisema: “Unajua kuna vitu vya kuandika, mimi sina taarifa na hilo.

“Huyo askari msaidieni asije akavunja sheria kwa kuleta masuala ya jeshi kwenu. Ukitaka kujua taarifa zake muulize mwajiri wake.”
 tunayo nakala ya barua UPEL.TRR ® Polisi (W) zote ® vikosi vyote TRR/A.24/5/Nyamongo/232, iliyosainiwa na SSP Sebastian Zacharia, ikiwaweka tayari askari hao kwa safari ya kwenda mgodini wakati huo.

Kwa mujibu wa nyaraka, viongozi wa kikosi hicho cha askari 31 walikuwa ni SGT Tabu, WP Vailet, PC Mauki, G9455 PC Hosea na D.2766 PC Andrew waliokuwa wakitumia gari ya polisi PT 1685.
Samwel alidai kuwa wakiwa kazini mgodini walishambuliwa kwa mawe na watu wasiojulikana na kuwasababishia majeraha sehemu mbalimbali za mwilli.

Alisema kutokana na tukio hilo, walifungua kesi M/NY/3032/10/2012 Oktoba 23, 2012, kuhusu shambulio hilo ambalo lilimjeruhi mkono wa kulia.

PC Samwel alisema kuwa alipewa barua na uongozi wa mgodi ili aweze kwenda hospitali ya Bugando.

Kwa mujibu wa Dk. Gerald Lenjima wa mgodi wa dhahabu wa Barrick uliopo Nyamongo, askari huyo alikuwa ameumia sana kiganja cha mkono wa kulia, na hivyo angehitaji uangalizi wa karibu wa madaktari bingwa.

Lakini mnadhimu wa jeshi hilo mkoani Mara alikataa ushauri wa daktari na kuamrisha apelekwe hospitali ya Shirati iliyopo mkoani humo.

Alisema kuwa baada ya kubaini kuwa mkono wake unaharibika, alienda kumwona Kamanda Kamugisha kuomba fedha za matibabu na nauli ili aweze kwenda Bugando kama alivyoandikiwa na daktari.

Daktari bingwa wa Bugando alielekeza kuwa PC Samwel ahudhurie matibabu ya mkono huo kwa wiki nane mfululizo kwa kuwa mifupa ilikuwa imevunjika.

Lakini Januari 21, 2012 aliomba ruhusa ili aweze kwenda Bugando kwa wiki nane na kujibiwa: ‘Umeamriwa kuondoka hapa kesho kwenda Bugando kwa ajili ya matibabu na umepewa siku tatu urudi hapa mara umalizapo matibabu.”

Chanzo chetu kilisema kuwa askari waliokuwa katika operesheni hiyo walikuwa wanalipwa na mgodi huo sh 25,000 kila mtu kwa siku, lakini Samwel baada ya kuumia aliacha kulipwa.

Samwel alisema kuwa akiwa katika hali hiyo ngumu, mkono wake ulibadilika rangi na hivyo akalazimika kufika tena ofisini kwa kamanda wa polisi kuomba ruhusa, fedha za nauli na matibabu aweze kurudi hospitali, lakini aliambulia matusi ya nguoni.

Kwamba alitishiwa kuwekwa mahabusu ya polisi kama mtuhumiwa kwa kumsumbua kamanda wa polisi, huku kamanda huyo akisema: “Nimekwambia jeshi halina fedha za kukutibu, unataka niuze gari ya kamanda ili nikupe nauli na fedha za kutibiwa?”

Baadaye alipewa ‘movement order’ ya kuruhusiwa kwenda hospitali kwa gharama zake na aliporudi na kupeleka maombi ya kulipwa fedha alizotumia kujitibu, alikataliwa akiambiwa hawana fedha.

Samwel aliongeza kuwa alipokwenda kwa kamanda alikamatwa na kuwekwa mahabusu na kupigwa marufuku ya kumwona bosi wake huyo na kuelezwa kuwa akirudia mkataba wake utazuiwa ili afukuzwe kazi.

0 comments:

Post a Comment